Sunday, February 20, 2011

Mpango wa MWAKEM: “Usiwe Jibu rahisi kwa tatizo kubwa !”

Dec, 16, 2010 taasisi ya uwezo Tanzania ilitangaza matokeo ya utafiti wake kuhusu uwezo wa watoto kusoma na kuandika nchini Tanzania. Katika utafiti huo, imebainika kuwa idadi kubwa ya watoto nchini hawawezi kufaulu majaribio kwa kiwango kilichotarajiwa. Matokeo ambayo kimsingi yanatoa wito wa kuboresha ufundishaji na ujifunzaji katika kila somo.


Kwa muda mrefu sasa, jamii imekuwa ikiwatupia mzigo mkubwa wa lawama walimu pindi ufaulu wa wanafunzi unapo kuwa duni. Kimantiki lawama hizo zinaweza kuwa na mashiko. Hii inatokana na ukweli kuwa ubora wa elimu itolewayo unategemea sana uwepo wa walimu wenye sifa,vifaa vya kufundishia na kujifunzia, mitaala thabiti na thahili,ushirikiano wa walimu, wanafunzi, wazazi,wadau wa elimu na tathmini sahii ya mtaala inayokubalika.

Kwa kutambua kuwa ubora wa walimu ni kigezo muhimu cha msingi katika kuinua ubora wa elimu, Wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ili kukidhi mahitaji katika utekelezaji wa mpango wa maendeleo ya sekta ya elimu (ESPP)ambao ilihusisha mipango kabambe ya MMEM na MMES iliandaa mkakati wa menejimenti na maendeleo ya walimu MMEMWA ili kuimarisha ubora wa elimu ya ualimu. Hii ilitokana na ukweli kuwa mafanikio ya mipango yote miwili MMEM na MMES litegemea sana upatikanaji wa walimu.

Aidha, kwa kutambua kuwa mafunzo ya walimu kazini ni nyenzo kuu ya kufanikisha ubora wa ufundishwaji na ujifunzaji darasani.Serikali imeamua kuimarisha programu za mafunzo kazini kwa walimu .Kuanzia Julai ,2010, wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ilianza kutekeleza mkakati wa mafunzo kazini kwa walimu wa shule za msingi ngazi ya shule-MWAKEM kwa lengo la kuinua ubora wa walimu wa shule za msingi katika kufundisha elimu ya awali na msingi kwa ufanisi.

Ni dhahiri kuwa ikiwa mpango huu utaratibiwa na kusimamiwa vema walimu watapata kujifunza mambo mapya kama vile mabadiliko ya mitaala, dhana na nadharia za ufundishaji na ujifunzaji na hivyo kuweza kukabiliana na changamoto za mabadiliko katika elimu kila wakati.

Kwa mujibu wa mwongozo wa usimamizi na utekelezajimwam MWAKEM uliotolewa novemba 2010,usimamizi na uendeshaji wa mafunzo kazini kwa walimu wa shule za msingi ngazi ya shule umeelekezwa vizuri sana.Aidha,watendaji wakuu katika utekelezaji huo na majukumu yao katika kila ngazi wameainishwa vema.Na kwa lengo la kuwa na mafunzo yenye ufanisi na endelevu kwa walimu mafunzo hayo yameandaliwa kutolewa kwa kushishikiana na halmashauri za wilaya.

Nashawishika kuuona mpango wa MWAKEM kuwa ni jibu rahisi kwa tatizo kubwa kwa sababu kuu mbili; mosi ni uzoefu unaotokana na utekelezaji wa mipango iliyotangulia na pili ni pengo kubwa lililopo kati ya ukweli wa hali ya elimu yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo katika kutathimini na kuinua ubora wa elimu nchini.

Utekelezaji wa mipango mingi ya maendeleo ya elimu iliyotangulia umekuwa na changamoto nyingi sana.Mfano mzuri katika kuelezea hili ni mpango wa mafunzo kazini kwa walimu wa daraja la tatu B/C-A mpango uliokuwa maarufu sana kwa jina la “moduli”. Utekelezaji wa mpango huo ulikumbana na changamoto nyingi sana.Kubwa miongoni mwa changamoto hizo ilikuwa ni utayari wa walimu tarajiwa kujiendeleza kuwa mdogo na halmashauri nyingi kutotenga fungu kwa ajili ya mafunzo kabilishi na yale ya ana kwa ana kati ya wakufunzi na walimu ili kutathimini maendeleo ya walimu katika kujifunzaji. Kwa mujibu wa mwongozo wa utekelezaji wa MWAKEM kila halmashauri imeelekezwa kutenga pesa kiasi cha tsh elfu arobaini [40,000/=] kwa kila mwalimu kwa ajli ya mafunzo hayo kila mwaka katika bajeti yake.Uzoefu unaonyesha kuwa halmashauri nyingi kipaumbele chao huwa sio maendeleo ya taaluma ya walimu na ndio maana mafungu hayo huwa hayapo na ikitokea yakatengwa huwa yanatumika kwa shughuli nyingine tofauti na malengo tarajiwa.Tatizo linaloonekana kuwa sugu.

Nimelazimika kutolea mfano mpango wa C/B-A na MWAKEM kwa kuwa wahusika wakuu katika utekelezaji wake ni wale wale na mfumo wa uendeshaji wake hauna tofauti na ule wa C/B-A ambao mafunzo yake yalitolewa kwa njia ya masafa kupitia moduli.

Sababu nyingine inayonifanya kuuona mpango huu ni jibu rahisi kwa taizo kubwa kama nilivyodokeza hapo awali ni pengo kubwa lililopo kati ya ukweli halisi wa hali ya elimu yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo katika kutathimini na kuinua ubora wa elimu nchini.Kwa mfano,ni ukweli usiopingika kuwa mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji darasani unategemea sana umahiri wa mwalimu.Ni udhaifu mkubwa ikiwa tutakuwa tunazungumzia mpango wa kumpata mwalimu “mahiri” pasipo kueleza njia na vigezo tutavyotumia katika kumpata na jinsi ya kumfanya auishi umahiri wake.

Napenda kuwakumbusha wadau na wanaharakati wa elimu kuwa ubora wa elimu ni zaidi ya kuwa na mwalimu “mahiri” kwani hutegemea sana uwepo wa mitaala thabiti na dhahiri,uwepo wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, walimu wenye sifa,miundombinu inayovutia ufundishaji na ujifunzaji na ushirikiano wa wazazi,walimu,wanafunzi na wadau wote wa elimu.

Aidha napenda kuwakumbusha pia kuwa pamoja na ukweli kuwa elimu yetu inachangamoto nyingi,bado mafunzo kazini kwa walimu ni ya lazima na yanayopaswa kuwa endelevu.Ikiwa mifumo ya uendeshaji na usimamizi itaimarishwa ni dhahiri kuwa kiwango cha ufundishaji wa walimu wetu kitaimarika na hivyo lengo la taifa la upatikanaji wa elimu bora kwa wote litafanikiwa.





MTOTO WA MKULIMA: Msamiati uliotekwa nyara!!!!!!

Harakati za ukombozi wa mwanadamu katika Nyanja zote za kiuchumi,kisiasa,kiutamaduni na kifikra zina historia ndefu.Kutokana hali hiyo ndiyo maana wanazuoni tunashawishika kuamini kuwa historia kwetu ni sasa ikivuviwa na zamani.Ni matendo ya sasa yakitiwa nguvu na yale ya waliotutangulia?!!

Nimeanza makala hii kwa maelezo hayo katika kuutafakari msamiati wa “Mtoto wa Mkulima” ili niweze kuonyesha pengo kubwa lililopo kati ya ukweli wa maisha yetu na jitihada za mantiki tunayotumia ili kuuona ukweli huo.

Msamiati wa “Mtoto wa Mkulima” umeshika kasi ya ajabu sana katika siku za hivi karibuni.Ulipoanza kutumika msamiati huu,watumiaji wake walikuwa wakimaanisha kweli wao ni watoto wa wakulima,watu safi,wenye kuenenda katika mapito safi na waliotayari kupigania maslahi ya wengi.Kutokana na hali hiyo,ndipo wafuasi lukuki wakajitokeza mstari wa mbele katika kuunadi msamiati huo.

Jumuia ya wanachuo wa chuo kikuu cha Dar es salaam ni moja ya maeneo ambayo msamiati wa mtoto wa mkulima umeshika kasi ya ajabu!!!!Wanazuoni kadha wa kadha wakijipambanua kama wanaharakati wamekuwa wakijinadi kama watoto wa wakulima ilihali kihalisia sio kweli-hawako hivyo hata kidogo!! Wamekuwa wakijitokeza mbele ya hadhira mikono nyuma wakiendeleza kile wanazuoni wanachokiita “Vuguvugu la Umajumuni” katika kupinga mifumo dhalimu inayotufanya kuafiki kile tusicho amini.Jambo la kusikitisha ni pale wanapopewa mamlaka/madaraka ya kuwaongoza wenzao ghafla hunaswa katika mikoba ya ya uchawi wa “Giningi” na kusahau kabisa misingi ya harakati zao na kisomo chao kilichowapa nafasi ya kuwa pale walipo. Wanaishia kufanya kinyume na kabisa matarajio ya watu na kuwaacha “ watoto wa wakulima” halisi wakiishi na tamaa zao katika hali ya kukata tamaa!!!?

Binafsi sishangai hali hii kutokea.Sishangai kwa kuwa ni hali niliyoitegemea.Ni hali iliyotegemewa kwa kuwa tangu enzi za uhuru wan chi hii waasisi wake walisema wazi kabisa kuwa hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.Baada ya wakulima kujipambambanua kuwa wao ni watu safi na wapiganaji katika ujenzi wa “Dunia bora kwa wote”, watoto wa wafanyakazi hasa wale wenye kipato kilichotukuka na kubatizwa majina yenye kuchukiza!? Hawakuwa na njia nyingine zaidi ya kuingia katika mduara na kujifanya nao ni wachezaji wa mdundo wa “Utenzi wa watoto wa wakulima”.Watoto wa wakulima wakadanganyika na kufikiri ni wenzao.Wanaposhituka,tayari wachezaji wakuu wa utenzi huo ni wale wale “waliotengwa”-hatimaye wametekwa nyara!!.Ishara ya hali hiyo ni matokeo ya utendaji wa viongo wetu ambao awali tulidhani ni wenzetu???!!!

Wanazuoni!!!! Ikiwa bado tunaamini katika misingi ya waasisi wa taifa letu ya kuwa hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.Basi huu ni wakati wetu muafaka kudurusu upya mantiki ya msamiati huu wa “ mtoto wa mkulima” ili kuupatia maana stahili katika wakati stahili. Katika kufanya hivyo ni budi tukajikita vema katika kuangalia vigezo tunavyovitumia kutambua motto wa mkulima au vinginevyo kama haja hiyo ipo na mantiki tunayoitumia katika kuwagawa “ watoto wa watanzania” katika madaraja/makundi hayo.

Binafsi, nafikiri huu ni wakati muafaka wa kuzungumzia “uzalendo” . Tuwazungumzie watoto wa wazalendo wa Tanzania [Wakulima: wadodo,wakati & wakubwa Na wafanyakazi: wa kima cha chini,kati na juu].Ikiwa msamiati wa “mtoto wa mkulima” tumekuwa tukilitumia kumpambambanua mtoto wa Mtanzania mwenye kipato cha chini basi hilo ni kosa kubwa ambalo hatuna budi kuacha kuendelea kulifanya haraka iwezekanavyo kwa kuwa sio kweli kuwa kila mtoto wa mkulima anatoka katika familia duni.Aidha,ikiwa msamiati huo tunautumia katka kuwapambanua “ wapiganaji” au wanaharakati wa vuguvugu la umajumuni basi huu ni wakati muafaka wa kutafuta msamiati sahihi baada ya msamiati wa “ mtoto wa mkulima kutekwa nyara!!!!.Hii ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.

Kazi ya mja kunena
Mungu ibariki Afrika,

Mungu ibariki Tanzania!!!!!

Mitaala yetu na hatma ya Elimu Tanzania.

Utekelezaji wa shughuli mbalimbali za serikali huongozwa na sear na kusimamiwa na sheria zilizoundwa kwa ajili ya kuhakikisha kuwa malengo yaliyokusudiwa yanafikiwa katika kiwango kilichotegemewa.Tangu uhuru,sekta ya elimu hapa nchini imeongozwa na sera mbili ambazo ni sera ya elimu ya kujitegemea na sera ya elimu na mafunzo ya 1995.

 Ujio wa sera ya elimu na mafunzo 1995 ilikuwa ni faraja kubwa sana kwa wadau wa elimu hapa nchini.Hii ni kutokana na ukweli kuwa sera hii ilileta mapinduzi makubwa sana katika sekta ya elimu ambayo hayajawahi kushuhudiwa tangu enzi za azimio la Arusha.Mapinduzi yaliyoletwa na sera hiyo ni kutokana na ukweli kuwa sera hiyo ilitokana na utafiti wa kina uliofanywa ili kutambua hali halisi ya elimu yetu na changamoto zake.Ujio wa sera hii ndio uliopelekea mabadiliko makubwa ya mitaala ya elimu yangu ya awali hadi elimu ya juu.

Miaka michache tu tangu kuingia na kuanza kutumika kwa mitaala hiyo iliyoandaliwa kwa misingi ya sera ya elimu na mafnzo ya 1995,nchi ilishudia mabadiliko mengine makubwa ya mitaala kwa kigezo chenye mashiko cha dhana ya “Ufundishaji unaozingatia ujenzi wa maana”.Haijulikanai ni utafiti kiasi gani ulifanyika ili kubaini udhaifu na ubora wa mitaala iliyokuwepo?! Kama hiyo haitoshi,mara tu baada ya mabadiliko hayo ya mitaala serikali kupitia wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi ikatangaza kufanyika kwa mabadiliko ya sera ya elimu-mswada unasubiri Baraka za bunge kuidhinishwa rasmi na kuwaacha wanazuoni midomo wazi na maswali mia kidogo;mathalani Mabadiliko ya sera na mabadiliko ya mitaala kipi kilipaswa kuanza? Je, ni utafiti kiasi gani umefanywa ili kujiridhisha kuwa sera ya elimu na mafunzo iliyopo haijatuletea tija na hivyo haitufai katika dunia ya “ulaji na uteja”[utandawazi na soko huria]? Ikiwa utekelezaji wa mitaala huongozwa na sera na kusimamiwa na sheria zinazoundwa ina maana kuwa mitaala yote iliyoandaliwa kati ya 2006 na 2008 na mingine kuanza kutumika rasmi 2009 itapaswa kubadilishwa ili kuenda sambamba na matakwa ya sera! Je, ni utashi gani tuliotumia kufanya haraka ya kubadili mitaala kabla ya kujua mahitaji halisi ya sekta ya elimu?Je, ikiwa hatukusudii kufanya mabadiliko makubwa katika sekta ya elimu hivi karibuni mswada wa sera ya elimu uliopo mezani una maana gani kwetu?Je, ubadilishaji holela wa mitaala pasipo kufanya upembuzi yakinifu ili kujua hali halisi ni matumizi sahihi ya pesa za wavuja jasho wan chi hii?Hakika maswali ni mengi ila majibu yanaweza kuwa ni mengi zaidi!.

Chimbuko la makala hii ni hofu iliyochipuka kutokana na mambo makubwa mawili;Kwanza ni ripoti ya tathimini kuhusu uwezo wa kujifunza katika elimu hapa nchini iliyotolewa na asasi ya Uwezo Tanzania na pili ni mabadiliko ya fedha yaliyotangazwa hivi karibuni.

Matokeo ya ripoti ya Uwezo Tanzania ni dhahili kuwa imewashitua watu wengi. Lakini kwa wafuatiliaji wa mabo hilo ni jambo lililotarajiwa na hali hiyo kihalisia inaweza kuwa ni mbaya zaidi ya matokeo ya utafiti huo. Aidha hofu yangu kutokana na mabadiliko ya pesa yaliyotangazwa hivi karibuni ni kutokana na ukweli kuwa mabadiliko hayo kwa namna moja au nyingine yanaweza kupelekea mabadiliko mengine ya mitaala hata kabla ya sera mpya ya elimu kuanza kutumika.Hii ni kutokana na ukweli kuwa fedha yetu ni moja ya alama za taifa letu na watoto wetu kwa kutumia mtaala uliopo wanajifunza juu ya alama hizo.Mfano,katika somo la hisababti darasa la tatu sura ya 3 mwanafunzi anajifunza kuhusu utambuzi wa fedha. Aidha katika darasa hilo hilo la 3 katika somo la Uraia sura ya 3 mada ya 6 anajifunza kuhusu fedha kwa lengo la kumwezesha mwanafunzi kutambua,kutathimini na kuheshimu alama za utambulisho wa taifa lake.Kwa mujibu wa muhtasari uliopo mwanafunzi anatarajiwa kufikia lengo tajwa hapo juu ikiwa ataweza kuainisha na kutaja alama zilizopo katika sarafu na noti za Tanzania.Noti zote zilizoainishwa katika mtaala huo ndizo zinazobadilishwa!!!Hii ina maana kuwa noti mpya na hizi zinazotumika sasa pamoja na kuwa na thamani sawa zitakuwa na alama zinazotofautiana.Kwa kuwa tumejifunza kukurupuka katika kufanya maamuzi,ni dhahili kuwa mihtasari hiyo itarekebishwa haraka ili kukidhi haja. Wakati zoezi hilo likikamika,sera mpya ya elimu itakuwa tayari na ni wazi kuwa maboresho mengine ya mtaala yatafuata!?Je ,katika hali kama hiyo tutarajie kitu gani? Je, ni lini mitaala yetu itatengemaa na hivyo kuwa na tahimini ya mtaala yenye mantiki? Je, ni nini hatma ya elimu yetu katika muktadha huu? Je, walimu,waelimisha walimu, watunga sera na wadau wengine wa elimu tunafanya nini katika hali hii?.